TATIZO LA WANAFUNZI 1280 KUKAA CHINI LIMEPATIWA UFUMBUZI NA MBUNGE WAO.


Ukosefu wa madawati  katika Shule ya Msingi Kilima A iliyoko Halmashauri ya Mji wa Kahama mkoani Shinyanga, huenda ukamalizika kufuatia Mbunge wa Jimbo la Kahama James Lembeli kuahidi kufuatilia magogo yaliyokamatwa na maliasili ili yatumike kutengenezea madawati.

Lembeli ameyasema leo alipokuwa mgeni rasmi kwenye Mahafali ya Darasa la saba ya shule hiyo, kufuatia Risala ya wanafunzi iliyosomwa kwake ikibainisha tatizo kubwa linalowakabili wanafunzi wa shule hiyo wapatao 1280, kuwa ni ukosefu wa madawati.

Katika Risala  hiyo, wanafunzi hao wamemwambia Lembeli kwamba  pamoja na idadi yao kubwa, shule ina madawati sitini yanayofanya kazi, ambapo kwa kawaida hukaliwa na wanafunzi Mia moja themanini huku wengine zaidi ya Elfu moja wakikaa chini.

Awali akitoa salam kwenye mahafali hayo, Diwani wa Kata hiyo Amosi Sipemba ameitaka serikali kuona umuhimu wa kutumia magogo ya miti yanayokamatwa na Idara ya Maliasili yatumike kutengenezea madawati katika shule hiyo.

Kufuatia ushauri huo, Lembeli ameahidi kutumia juhudi zake zote kuwasiliana na idara ya maliasili ili magogo hayo yatumike kutengeneza madawati hayo huku akiahidi kugharamia matengenezo yake yote.

Lembeli pia ameahidi kuchangia bati 60 kwa ajili ya kuongeza vyumba vya madarasa katika Shule hiyo, kitu ambacho amekuwa akikifanya jimboni mwake, ili kuwahamasisha wananchi kuchangia nguvu zao katika shughuli za maendeleo.

0 comments: